Ushirikiano wa UNCDF na wananchi wa Ikungi Tanzania waleta mabadiliko chanya

#HabarizaUN #UmojawaMataifa #Kiswahili #UNNewsKiswahili #UNCDF Kuanzia wiki hii viongozi wa ulimwengu wanamiminika jijini New York Marekani kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa kushiriki Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa. Mambo kadhaa yatajadiliwa ikiwemo amani, haki za binadamu, uchumi na kuilinda sayari dunia dhidi ya uharibifu unaochochea majanga. Ulimwengu tayari umebaini kuwa changamoto zimefungana na hivyo majawabu yanapaswa kutafutwa kwa kushirikiana. Katika maeneo ambayo ushirikiano umefanyika ili kutafuta ufumbuzi wa jambo, matunda yameonekana. Mathalani nchini Tanzania, shirika la mitaji la Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na wananchi wa wilaya ya Ikungi, mkoani Singida, wanaendelea na mradi wa kutatua changamoto ya umeme na maji, masuala mtambuka ambayo yanagusa sekta nyingine kama elimu, afya, uchumi na mazingira. Mradi wa umeme wa nishati ya jua kupitia ufadhili wa shirika la mitaji la Umoja wa Mataifa, UNCDF umeanza kuzaa matunda kwa wananchi kama anavyosimulia Jongo Sudi wa redio washirika Ruangwa FM.
Back to Top